Mafunzo ya Wanachama Wapya wa Mtandao wa watetezi wa Haki za Binadamu Yafunguliwa Rasmi Mkoani Dodoma

Mtandao wa watetezi wa haki za binadamu -THRDC  wenye wanachama zaidi ya 300 waandaa mafunzo kwa watetezi wa haki za binadamu ambao ni wanachama wake wapya kutoka kanda zake  zote   11 nchini Tanzania.

Mafunzo haya  yanafanyika kwa siku mbili mkoani dodoma kuanzia Tarehe 17 mpaka tarehe 18 Machi 2025 yakilenga kuwajengea uwezo wanachama hao katika  masuala ya usalama, kanuni na taratibu za mtandao, namna bora ya kuripoti matukio ya ukiukwaji wa haki za binadamu na  uzingatiaji wa sheria.

Katika kutoa salamu  na ukaribisho, Mratibu wa kitaifa  wa mtandao wa watetezi Tanzania wakili Onesmo  Olengurumwa aliweza  kuwapongeza  wanachama hao wa THRDC kwa maamuzi na utayari  wa kujiunga  na mtandao kwani hii inaonyesha wazi kuwa kazi zinazofanywa na Mtandao huu zinaonekana na ni dhahiri  kuwa zinaigusa jamii  moja kwa  moja.

THRDC imefanya kazi kubwa kuhakikisha watetezi wa haki  za binadamu wanatambulika nchini na kuweza kufanya kazi kwa karibu na serikali katika  kulinda na kutetea haki za binadamu nchini.

Aliongeza kuwa kama mtandao, THRDC ina sera kanuni na taratibu zake kwa wanachama  wake , hivyo ni mihimu kwa wanachama wote kuzifahamu kiundani, kuelewa sheria za nchi zinazosimamia Mashirika na kuzifuata (compliance)

Alisisitiza kuwa watetezi wa haki za binadamu  wanapaswa kufanya utetezi kwa kuzingatia sheria na kanuni  zote za nchi na  kutumia namna bora ya kufanya  utetezi bila kusahau njia  njia na mbinu sahihi za   kajilinda na  changamoto za kiusalama zonazotokana  na  kazi zao za utetezi.

Katika ufunguzi wa  Mafunzo haya, mgeni rasmi  ambae ni Raisi wa chama cha wanasheria Tanzania wakili Boniface Mwambukusi alisisitiza kuwa  kazi ya utetezi wa haki za binadamu sio kazi rahisi Bali ni kazi ya  wito na kujitoa kwa moyo kwani watetezi wa haki za Binadamu ni sauti kwa wasio na sauti, ni macho kwa wasio na macho na ni nuru ya haki kweye giza la dhulma.

Alikazia kwa kusema kuwa suala la utetezi wa haki za binadamu sio kosa la jinai  bali ni suala la kikatiba na la kimataifa kwani Tanzania imeridhia mikataba Mingi ya kimataifa ya haki za binadamu isipokuwa michache.

Alimaliza hotuba yake kwa  kuishukuru THRDC kwani imekuwa msaada mkubwa  kwake na imekuwa ikimsaidia  na kumtetea mara nyingi kila alipokuwa anapitia changamoto katika harakati zake za utetezi wa haki  na usimamizi wa sheria.

Wakili Mwambukusi alimaliza kwa kutoa wito kwa watetezi kutimiza wajibu wao na kusshirikiana  na serikali katika kufanya ushawishi wenye tija  (advocacy) kuanzia ngazi za chini za vijiji mpaka ngazi za juu za wafanya maamuzi bila kusahau kutetea haki za wanaume  kama ilivyo kasi katika kutetea haki za wanawake, kwani kuwaacha wanaume nyuma katika utetezi  kunapunguza kasi ya kufikia malengo  ya haki na usawa  hata katika jamiii.

Mtandao wa Watetezi wa Haki. Za Binadamu - THRDC
17 March 2025