THRDC YAFANYA MAFUNZO YA SIKU MBILI YA ELIMU YA SHERIA KWA WANASHERIA WA HAKI ZA BINADAMU NCHINI TANZANIA

Leo tarehe 27 Juni 2025, Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), kwa kushirikiana na EALS,  ZAFELA, PALU na TLS kupitia mradi wa SCATZ unaofadhiliwa na Umoja wa ulaya (EU), umeanza rasmi mafunzo ya siku mbili ya elimu ya sheria kwa wanasheria wa haki za binadamu nchini Tanzania. Mafunzo haya yanafanyika katika Hoteli ya Morena jijini Dodoma.


Mafunzo haya yamewakutanisha wanasheria na mawakili  zaidi ya 50 kutoka maeneo mbalimbali ya nchi  pamoja na wawasilishaji wa mada wakiwemo  majaji wastaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania kama Mh. Jaji Robert Makaramba na Mh. Jaji Fauz Twaibu sambamba na  viongozi mbalimbali wa vyama na jumuia za  wanasheria wakiwemo viongozi kutoka TLS,  EALS, ZAFELA na PALU yakiwa ni   muendelezo wa mpango  wa THRDC katika kutoa elimu endelevu ya haki za binadamu (CLE) kwa wanasheria na mawakili   nchini Tanzania. 


Lengo kuu la mafunzo haya ni kuimarisha uwezo wa wanasheria nchini ili kuhakikisha upatikanaji wa haki unaozingatia misingi ya haki za binadamu, kupitia matumizi bora ya sheria za kitaifa, kikanda na kimataifa, huku wakizingatia utawala wa sheria, maadili ya taaluma. 


Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo haya, Wakili Onesmo Olengurumwa - Mratibu wa Kitaifa wa THRDC, alisisitiza kuwa mafanikio katika kulinda haki za binadamu  na utawala bora yanahitaji ushirikiano kati ya asasi za kiraia, jumuia/vyama vya wanasheria, na serikali jambo ambalo mradi huu wa SCATZ na kutiliwa mkazo. Aliongeza kuwa kuelekea Uchaguzi mkuu wa 2025, ni muhimu kwa wanasheria kutambua wajibu wao katika kuchambua na kushughulikia changamoto za kisheria zitakazojitokeza kabla, wakati na baada ya uchaguzi.


Mafunzo haya pia yanatoa fursa ya kipekee kwa washiriki kujadili masuala muhimu kama vile dhana ya mashauri ya maslahi ya umma (PIL),  nafasi ya vyama vya wanasheria katika kuendeleza kesi hizo, matumizi ya mikataba ya haki za binadamu  katika kulinda haki za wananchi, pamoja na masuala ya maadili ya wanasheria katika matumizi sahihi  ya teknologia na  mitandao ya kijamii kwenye dunia ya sasa ya kidijitali.


THRDC

27 Juni 2025